Alhamisi , 6th Aug , 2015

Azimio jipya la ulipaji faini kwa njia ya mtandao limejadiliwa na kuazimiwa na wajumbe wa mkutano Mkuu wa wadau wa usalama barabarani ili kuweza kupunguza ajali za barabarani katika kuelekea kwenye maadhimisho ya wiki ya nenda kwa usalama barabarani.

Kamanda wa kikosi cha Usalama barabarani nchini Mohamed Mpinga.

Makubaliano hayo yamekuja mara baada ya agizo lililotolewa na Rais wa Tanzania Dkt, Jakaya Kikwete juzi katika uzinduzi wa wiki ya nenda kwa usalama barabarani.

Akizungumza na waandishi wa habari Kamanda wa kikosi cha Usalama barabarani nchini Mohamed Mpinga ameeleza kuwa katika kutekelza moja ya maagizo aliyoyatoa Rais Kikwete lakini pia wamejadiliana na kukubaliana kuwa ipo haja ya kuwa na ushirikiano na wadau wengine wakiwemo watu binafsi ili kukamilisha suala hilo.

Nae Naibu Waziri wa Mambo ya ndani Perreira Sirima amesema mafunzo pekee kwa madereva na waendesha vyombo vya moto hayawezi kusaidia na badala yake mamlaka mbalimbali zinazohusika zisimamie sheria vyema na kuweza kuzifanyia marekebisho sheria hizo.

Kwa upande wake Idd Azan ambae ni mjumbe wa baraza hilo na mbunge wa jimbo la kinondoni amesema sheria hiyo itapunguza manung'uniko kwa madereva na watumiaji wa vyombo vya moto kuwa pesa hizo zitolewazo kama faini huwa ni mradi wa askari na badala yake kuwa na uhakika wa pesa hiyo kuingia katika mfuko wa serikali pamoja na watumiaji wa vyombo vya moto kuziheshimu sheria za usalama barabarani.

Mkutano Mkuu uliofunguliwa na mwenyekiti wa baraza la usalama barabarani uliofanyika kwa siku mbili kwenye ukumbi wa Regal Naivera jijini Tanga umemalizika ambapo umeweza kujumuisha wajumbe mbalimbali wa ndani na nje ya nchi ili kuweza kujadiliana namna ya kupunguza ajali za barabarani ambazo hupunguza nguvu kazi ya Taifa.