Jumatano , 24th Feb , 2016

Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP) leo limeadhimisha miaka 50 tangu lilipoanzishwa lengo lake kuu likiwa ni kusaidia kupambana na kuondoa umasikini, kupunguza kutokuwepo kwa usawa na ubaguzi.

Katika taarifa yake aliyoituma kwa vyombo vya Habari katika maadhimisho hayo Mwakilishi Mkazi wa UNDP nchini Tanzania Bw. Alvaro Rodriguez amesema shirika hilo lilianza kutoa misaada nchini Tanzania mwezi Mei mwaka 1978 na tangu wakati huo limeendelea kushirikiana na serikali katika kufanikisha agenda yake ya maendeleo.

Mwakilishi huyo Mkazi amesema shirika la UNDP ambalo kwa sasa linafanya kazi katika nchi 170 duniani, limeendelea kushirikiana na serikali kuiwezesha kuratibu misaada ya kimataifa kimikakati na utekekelezaji wa mipango mbalimbali na kuimarisha mifumo ya kiutawala na kiuongozi.

Kwa upande wa utawala kidemokrasia UNDP imeendelea kutoa mafunzo kwa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Baraza la Wawakilishi Zanzibar.