Ijumaa , 29th Jul , 2016

Waziri wa Nishati na Madini Prof. Sospeter Muhongo, amewataka viongozi wote wa Mikoa na Wizara washirikiane kwa pamoja katika kusimamia miradi mbalimbali ikiwemo ujenzi wa mabomba makubwa ya usafirishaji ili kukuza uchumi wa nchi kupitia miradi hiyo.

Waziri wa Nishati na Madini Prof. Sospeter Muhongo.

Hayo yamebainishwa leo Jijini Dar es Salaam, na Waziri wa Nishati na Madini Prof. Sospeter Muhongo, wakati wa ufunguzi wa Semina ya wakuu wa mikoa na makatibu wakuu wa wizara juu ya usimamizi wa miradi inayotekelezwa na wizara ya Nishati na madini.

Prof.Muhongo amesema endapo nchi ikitaka kufikia Malengo ya kuwa nchi ya kipato cha kati mpaka ifikapo mwaka 2025 basi hakuna budi kwa taasisi zote kushirikiana kwa ukaribu pamoja na wananchi katika kusimamia miradi ya Maendeleo.

Prof.Muhongo amesema kuwa serikali inafanya kila jitihada ya kukamilisha bomba la mafuta kutoka Uganda hadi Tanzania, lakini pia ipo katika mpango wa kusambaza mabomba ya gesi nchi nzima ili nishati hiyo iweze kuwanufaisha Watanzania wengi zaidi kwa kukuza uchumi wa nchi na mtu mmoja mmoja.

Aidha Prof. Muhongo ameongeza kuwa Serikali inaendelea kufanya utafiti wa kutafuta rasimali ya mafuta na gesi katika maeneo tofauti ambapo kwa sassa wanampango wa kujadiliana na Congo(DRC), juu ya kufanya utafiti wa rasilimali hiyo ndani ya ziwa Tanganyika.

Sauti ya Waziri wa Nishati na Madini Prof. Sospeter Muhongo.