Jumatano , 30th Dec , 2015

Wakulima wa mikoa ya Lindi na Mtwara wameshauriwa kutumia teknolojia ya mifuko ya PICS inayotumika kuhifadhia mazao, kama njia bora ya kuyakinga ili yasiharibiwe na wadudu na kuachana na kutumia njia ya kemikali ambayo inaweza kuleta athari baadae.

Mkuu wa Wilaya ya Mtwara Fatma Salum Ally

Akizungumza mkoani Mtwara katika semina ya kuwajengea uwezo wadaau wa kilimo juu ya matumizi ya teknolojia hiyo, mkuu wa wilaya ya Mtwara, Fatma Ally, amesema wakulima wengi hapa nchini wanakumbwa na changamoto ya upotevu wa mazao baada ya mavuno, na ndio wanaoathirika kwa kiasi kikubwa ukilinganisha na serikali.

Aidha, amesema uwepo wa mifuko hiyo umetokana na kuwepo kwa wadudu waharibifu wanaoshambulia mazao ghalani hasa Dumuzi ambao uharibu mazao ya wakulima masikini katika nchi zinazoendelea, na kuwakwamisha wakulima wanaotegemea mazao hayo kwa chakula na biashara ili kuongeza kipato katika kaya zao.

Kwa upande wake, mshauri mwelekezi wa mradi huo ambao ulianza kufanya kazi mwaka 2014, Bernadetha Majebele, amesema mradi huo una malengo kadhaa kwa wakulima ikiwa ni pamoja na kuwafanya wakulima wadogo kujua namna ya kuhifadhi chakula chao na kukitumia baadae, na kuwatoa watanzania katika matumizi ya kemikali katika kuhifadhi mazo kwasababu ina athari kiafya.