Ijumaa , 13th Sep , 2019

Mara baada ya Mtihani wa Darasa la Saba kumalizika siku ya Alhamisi ya Septemba 12, Jeshi la Polisi Mkoa wa Kagera, limetoa taarifa ya uwepo wa udanganyifu wa mtihani huo kwa baadhi ya shule za mkoani humo.

Akizungumza leo Septemba 13, 2019, Kamanda wa Polisi Mkoani humo ACP Revocatus Malimi, amesema kuwa hadi sasa jeshi hilo,  linawashikilia Walimu 10  kwa tuhuma za wizi wa mitihani katika Shule ya Msingi Kumunazi Wilayani Ngara.

Kamanda Malimi amesema kuwa,Walimu hao walikutwa wamejifungia kwenye nyumba ya mmoja wa walimu, huku wakiandaa majibu ya somo la Sayansi, tukio ambalo linawajumuisha Walimu wa Shule hiyo pamoja na Walimu wasimamizi, walioteuliwa kusimamia mtihani huo.

''Kitendo kilichofanywa na watuhumiwa hao ni kosa la jinai kwani, mitihani mbali kuwa ni kipimo cha kuwaandaa na kuwapata wataalamu wa baada ni siri kuu  ya nchi, licha ya kupewa semina na kula kiapo cha uadilifu ikithibitika wamehusika na udanganyifu wa aina yoyote wakifikishwa mahakamani adhabu yake  ni  kubwa'' amesema ACP Malimi.

Aidha Kamanda Malimi amesema, bado wanaendelea na upelelezi na pindi utakapokamilika watafikishwa mahakamani.