Jumatatu , 15th Feb , 2016

Serikali imewaagiza wakurugenzi watendaji wa halmashauri zote nchini kuchukua hatua kali ikiwa ni pamoja na kuwafukuza kazi watumishi wa idara ya ardhi ambao wamebainika kujihusisha na vitendo vya rushwa.

Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya makazi mhe. Angelina Mabula.

Agizo hilo limetolewa mjini Musoma na Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi mhe. Angelina Mabula, wakati akizungumza katika kikao cha majumuisho ya ziara yake ya kukagua shughuli mbalimbali za wizara yake mkoani Mara ambapo amesema hatua hiyo imetajwa kuchangia migogoro mingi ya ardhi katika maeneo yao.

Bi. Angelina amesema serikali imebaini kuwa migogoro mingi ya ardhi imechangiwa kwa kiasi kikubwa watumishi wa idara hiyo kwa maslahi binafsi.

Kwa upande wake mkuu wa wilaya ya Bunda, Bw. Joshua Mirumbe, amewataka wananchi wote ambao tayari wamelipwa fidia kwa ajili ya kupisha eneo uwekezaji wa kiuchumi (EPZ), kuondoka mara moja kabla ya serikali haijachukua hatua za kuzivunja nyumba hizo.

Naye katibu tawala wa mkoa wa Mara, Bw.Benedict Ole Kuyani ameiomba serikali kutoa fedha za uendeshaji wa mabaraza ya ardhi hatua ambayo amesema itasadia kutatua migogoro mingi ya ardhi mkoani Mara.

Aidha kamishina wa ardhi kanda ya ziwa, Bw. Joseph Shewiyo, akizungumza katika kikao hicho ambacho kimeshirikisha viongozi na watendaji wa halmashauri za mkoa wa Mara, ameagiza halmashauri zote kusimamia sheria kwa kubomoa nyumba zote ambazo zimejengwa baada ya mwezi mei mwaka 2001 ndani ya mita sitini katika maeneo ya fukwe za ziwa, mito, maneo ya wazi na hifadhi za barabara.