Ijumaa , 19th Apr , 2019

Watuhumiwa wanne wamefikishwa katika Mahakama ya Kisutu wakituhumiwa kwa makosa manne ya matumizi mabaya ya mtandao ikiwemo kutapeli wananchi kupitia ukurasa wao wa Facebook.

Mke wa Rais Magufuli Mama Janeth.

Washtakiwa hao wamekuwa wakitoa mikopo kupitia Taasisi waliyoitaja kuwa ni ya Mama Janeth Magufuli, pia wanakabiliwa na shtaka la kutakatisha fedha kiasi cha shilingi milioni 4.5. Washtakiwa hao wametambulika kwa majina ya Saada Uledi, Maftaha Shabani, Heshima Ally na Shamba Baila.

Akisoma hati ya mashtaka, wakili wa serikali Batilda Mushi alidai washtakiwa hao kwa pamoja wanakabiliwa na kesi ya uhujumu uchumi namba 30/2019.

Alidai shtaka la kwanza ambalo ni kula njama, washtakiwa kwa pamoja wanadaiwa kuwa kati ya Januari 2017 na Machi 2019 katika jiji la Dar es salaam walichapisha taarifa za uongo kupitia akaunti yao ya mtandao wa kijamiii wa Facebook.

Shtaka la pili, washtakiwa wanadaiwa siku na eneo hilo walichapisha machapisho katika akaunti yao ya mtandao wa kijamii wa Facebook, wakionyesha Janeth Magufuli ambaye ni mke wa Rais  Magufuli ameunda taasisi ya kutoa mikopo kwa watu mbalimbali ikiwa na masharti ya kuweka fedha kabla ya kupewa mkopo kama ni kinga ya mkopo huku wakijua kuwa ni uongo.

Shtaka la tatu, wanadaiwa Machi 2 na 8 mwaka huu jijini Dar es Salaam, wakiwa kama waendeshaji wa akaunti hiyo ya Facebook, walisajili akaunti hiyo kwa jina la Janeth Magufuli kwa nia ya kudanganya na kujipatia Sh 4,487,000 kutoka kwa Paul Kunambi kama kinga  ya mkopo wakati wakijua kuwa siyo kweli.

Baada ya washtakiwa hao kusomewa mashtaka yanayowakabili, Hakimu Kasonde alisema hawatakiwi kusema chochote mahakamani hapo kutokana na kesi inayowakabili kuwa ni ya uhujumu uchumi.

Upande wa mashtaka ulieleza kuwa upelelezi wa kesi hiyo bado haujakamilika hivyo wanaomba tarehe nyingine kwa ajili ya kutajwa. Hakimu Kasonde aliahirisha kesi hiyo hadi Mei 2, 2019 itakapotajwa na washtakiwa wamerudishwa rumande kutokana na kesi inayowakabili kutokuwa na dhamana.