Jumapili , 15th Jan , 2023

Watu zaidi ya 40 wanasadikika kufariki dunia kwenye ajali ya ndege ya Shirika la Yeti iliyoanguka leo karibu na uwanja wa ndege wa Pokhara nchini Nepal. Ndege hiyo iliyokuwa na watu 72 ilikuwa inatoka Kathmandu kuelekea mji wa kitalii wa Pokhara, imeanguka wakati inatua na ikalipuka moto.

Wanajeshi wa jeshi la anga nchini Nepal wakiendelea na shughuli za kuopoa miili ya wahanga wa ajali

Video iliyotumwa kwenye mitandao ya kijamii inaonesha ndege ikiruka chini kwenye eneo lenye watu wengi kabla ya kupata adha hiyo. Kulikuwa na abiria 68 ndani ya ndege hiyo, wakiwemo angalau raia 15 wa kigeni, na wafanyakazi wanne.

Wanajeshi 200 wa Nepal wanahusika katika uokoaji katika eneo la ajali kwenye korongo la Mto Seti, kilomita moja na nusu tu kutoka uwanja wa ndege. Video ya eneo la ajali inaonesha moshi mnene unaofuka na uchafu unaowaka.

Waziri Mkuu Pushpa Kamal Dahal ameitisha kikao cha dharura cha baraza lake la mawaziri na kuvitaka vyombo vya dola kufanyia kazi shughuli za uokoaji.

Kati ya abiria hao, 53 wanasemekana kuwa Wanepali. Kulikuwa na Wahindi watano, Warusi wanne na Wakorea wawili kwenye ndege. Pia kulikuwa na abiria mmoja kutoka Ireland, Australia, Argentina na Ufaransa miongoni mwa wengine.