Jumanne , 3rd Dec , 2019

Watu watatu akiwemo Dereva na utingo wake, wamefariki Dunia baada ya Gari kubwa la kusafirishia mafuta, kufeli breki na kuligonga gari jingine katika kijiji cha Ibula,wilayani Rungwe, mkoani Mbeya.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mbeya, Ulrich Matei.

Kamanda wa Polisi mkoani hapo, Ulrich Matei, amesema ajali hiyo iliyohusisha gari aina ya Howo, mali ya Kampuni ya Camel Oil, lililokuwa na tera lake likielekea nchini Malawi, imetokea leo Desemba 3, 2019, majira ya saa 4:00 asubuhi, katika eneo la Kanyegele maarufu kama Airport, Kata ya Kiwira, wilayani Rungwe.

Kamanda Matei amewataja waliopoteza maisha kuwa ni Frank Chota (48), ambaye ni Dereva wa gari la kusafirishia mafuta, pamoja na utingo wa gari hilo aliyefahamika kwa jina moja la Silas,wote wakazi wa Morogoro.

Mwingine ni Nelson Samson (35), ambaye ni Dereva wa gari ya kampuni ya maji ya Rungwe Spring na mkazi wa Airport jijini Mbeya.

Kwa mujibu wa kamanda Matei, chanzo cha ajali hiyo ni hitilafu kwenye mfumo wa breki wa gari lenye tanki la mafuta na kupelekea tairi moja la nyuma kushika moto na kwamba miili ya marehemu imehifadhiwa katika Hospitali ya Wilaya ya Rungwe – Makandana.