Jumatatu , 5th Sep , 2022

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa, amewataka Watanzania walioajiriwa katika mradi wa ujenzi wa barabara ya mzunguko wa nje wa jiji la Dodoma, kuwa walinzi wa vifaa vinavyotumika kwenye ujenzi na kuwataka wahakikishe vifaa vinabaki salama.

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa

Kauli hiyo ameitoa wakati alipokagua maendeleo ya ujenzi wa mradi wa barabara ya mzunguko wa nje wa jiji la Dodoma, ikiwa ni sehemu ya mradi  wa uendelezaji wa jiji hilo.

"Pambaneni na wote wenye nia ya kuiba vifaa hivi, tunataka tupate barabara yenye viwango," amesema Waziri Mkuu

Aidha, waziri Mkuu ameitaka Wakala ya Barabara Tanzania (TANROADS) kwa kushirikiana na Ofisi ya Rais TAMISEMI, kuweka utaratibu wa kuwaweka pamoja vijana ambao wanashiriki kwenye ujenzi wa miradi mbalimbali nchini ili waweze kutumika zaidi kwenye makampuni ya ujenzi ya wazawa.

Ujenzi wa barabara hiyo yenye urefu wa kilomita 112.3 unafadhiliwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB).