Jumamosi , 16th Dec , 2017

Kiongozi wa chama cha ACT Wazalendo na Mbunge wa Kigoma mjini Zitto Kabwe amesema wanachama wa Chama hicho waliohamia Chama cha Mapinduzi (CCM) sio kweli wanaunga mkono juhudi za Rais bali ni kwaajili ya madaraka na ahadi walizopewa.

Hayo ameyasema leo kwenye hotuba yake kwa Kamati Kuu Juu ya chama hicho juu ya Hali ya Siasa Nchini Tanzania. Mh. Zitto ameeleza kuwa hoja inayotolewa na wanachama wanaohama ACT Wazalendo ya kuunga mkono jitihada za Rais haina mashiko kwani walikuwa na nafasi ya kuunga mkono wakiwa ndani ya chama hicho.

"Takribani watu wote wanaoondoka kutoka vyama vya upinzani kwenda chama tawala wanasema wanaunga mkono juhudi za Mwenyekiti wa Chama Tawala katika uendeshaji wa nchi yetu. Hii sababu haitoshi kueleza maamuzi yao, hususani kwa wale wanaotoka chama chetu cha ACT Wazalendo", amesema Zitto.

Kiongozi huyo wa Chama ameongeza kuwa Halmashauri Kuu ya Chama iliyooketi katika ukumbi wa Jeshi la Wokovu, Aprili, 2016 iliazimia masuala ambayo chama hicho kinaweza kuunga mkono ikiwemo mapamabno dhidi ya Ufisadi.

"Ni dhahiri kuwa wenzetu wana sababu zaidi ya kumuunga mkono Rais, kuna ambao sababu ni vyeo walivyopewa, na wengine ahadi za vyeo watakavyopewa", amesema Zitto. 

Chama Cha ACT Wazalendo hivi karibuni kimeondokewa na wanachama wake waandamizi ambao ni Profesa Kitila Mkumbo, Anna Mghwira, Albert Msando, Samson Mwigamba na Edna Sunga. Wote wamejiunga na CCM.