Alhamisi , 9th Aug , 2018

Msanii wa muziki wa kizazi kipya ambaye ilisemekana yupo kwenye mahusiano ya kimapenzi na muigizaji wa vichekesho Ebitoke, ameweka wazi juu ya mahusiano yao kwamba walishindwa kuwa wapenzi kutokana na mmoja wao kutokuwa muwazi kwa mwenzake.

Ben Pol amebainisha hayo wakati alipokuwa anazungumza kwenye kipindi cha KIKAANGONI kinachorushwa mubashara kupitia ukurasa wa kijamii wa facebook wa EATV, baada ya miongoni mwa shabiki zake waliokuwa wakimfuatilia, alipotaka kufahamu undani wa mahusiano yake na Ebitoke.

"Kiukweli sijawahi kuwa na mahusiano na Ebitoke na wala ile haikuwa kiki. Kilichotokea ni kwamba hatukufanikiwa kuwa na mahusiano licha ya wananchi au mashabiki zangu wenyewe kumpitisha kuwa mpenzi wangu kabla ya mimi sijamuona na kumkubali", amesema Ben Pol.

Pamoja na hayo, Ben Pol ameendelea kwa kusema "Ebitoke alikubarika hadi kwa wazazi wangu kutokana na yeye kuonekana kwenye vyombo vya habari akidai mimi ni mpenzi wake. Wazazi wakawa wanajua kwamba wameshapata mkwe wao. Hapakuwa na mapenzi ya kweli baina yetu ila tulikuwa tunafanya vile ili kuwaridhisha mashabiki zetu".

Mbali na hilo, Ben Pol amesema chanzo cha mapenzi hayo kushindwa kuendelea ni kutokana na Ebitoke kuogopa kusema ukweli.

Kati kati ya mwaka 2017, Ebitoke kwa mara ya kwanza aliweka hadharani hisia zake za kimapenzi juu ya msanii Ben Pol, lakini kwa bahati mbaya alishindwa kueleweka kwa haraka kwa jamii, kutokana na muonekano wake ambao watu walimzoea kumuona na kupelekea kudharauliwa huku wengine wakimshauri atafute mwanaume wa aina yake.

Juni 25 mwaka 2017, Ben Pol kupitia mitandao ya kijamii alimwagia sifa Ebitoke ikiwa kama ishara ya kukubali ombi la mwanadada huyo kuwa naye kimahusiano licha ya kuwa ukweli wa kila kitu walikuwa wanaufahamu wenyewe.

Mtazame hapa chini Ben Pol akifunguka mengine zaidi..