Ijumaa , 16th Aug , 2019

Sekta ya burudani imekumbwa na msiba wa kuondekewa na mmoja wa wasanii anayeunda kundi la The Mafik aitwaye Mbalamwezi, kilichotokea usiku wa kuamkia leo.

Msanii wa The Mafik, Mbalamwezi (katikati), aliyefariki dunia

Akizungumza na EATV & EA Radio Digital Hamadai ambaye anaunda kundi hilo
amesema taarifa za kifo chake alizipata jana jioni, ambapo kabla ya taarifa hizo tayari walikuwa wakimtafuta kwa siku tatu bila mafanikio.

"Taarifa za kifo chake nilizipata jana jioni. Kabla ya kifo chake hakuonekana kwa siku tatu, Hapa nilipo siwezi nikatoa taarifa zilizonyooka kwa sababu kifo chake kinahitaji maelezo, Nipo katika utaratibu wa kupata mwili wa ndugu yangu", amesema Hamadai.

Aidha mmoja wa meneja wanaolisimamia kundi la The Mafik amesema yupo njiani akielekea hospitali kuthibitisha ila taarifa hizo ni za ukweli na sababu ya kifo chake hakijatokana na ajali wala kuumwa kwakuwa hakuwa anasumbuliwa na ugonjwa wowote.

Pia baadhi ya ndugu wa marehemu wamesema taarifa waliyoipata kutoka kwa wasanii wenzake kuwa walimkuta  hana nguo na wanafuatilia polisi kwa ajili ya uchunguzi zaidi.

Msanii huyo ameshiriki katika kazi za kundi ambazo zimefanya vizuri kama Passenger, Sheba,Carola, Vuruga, na Dodo pia ameshirikiswa katika nyimbo za Ruby na Ben Pol.