Jumatatu , 11th Feb , 2019

Msanii wa Bongo Fleva, Peter Msechu amesema pamoja na kufanya mazoezi ya kupunguza unene ila hatathubutu kupunguza tumbo lake kwa kuwa ndio utambulisho wake, hivyo anapambana kupunguza kichwa, miguu, shingo, kifua na si tumbo. 

Peter Msechu

Akizungumza na eNEWZ, Peter Msechu amesema mabadiliko hayawezi kuonekana mapema kama mtu hafuatilii kwa makini kwa kuwa ameanza mazoezi tangu mwezi Machi mwaka uliopita.

Amesema alikuwa na kilo 132 ila kwa sasa ana kilo mia moja na kumi na watu hawajui kuwa anafanya mazoezi kwa afya lakini kitu ambacho hatoweza kupunguza ni tumbo lake na wala hafanyi mazoezi ili kupunguza tumbo.

"Nitapunguza kila kitu ila tumbo sipunguzi, nitapunguza hipsi miguu, kichwa, kifua, lakini tumbo nalimaintain pale pale kwa sababu ndio silaha,  tumbo ni rahisi zaidi kuliongeza kuliko kulipunguza mimi nagonga wali maharage linazidi kurefuka tu na sijafeli kulipunguza kama watu wanavyosema na watu wasione nafanya 'gym'".

"Wajuwe nataka kupunguza tumbo halafu kwanza hakuna anayenipa hela ya gym", amesema Peter Msechu.

Hata hivyo amemaliza kwa kusema kuwa harusi yake atafunga baada ya miaka mitano kwa kuwa anasubiri pete aliyomvisha mpenzi wake ichakae ndio maana amekuwa kimya na anafikiri kumuoa mpenzi wake huyo baada ya miaka mitano kwa kuwa tayari ameshakaa nae kwa miaka sita, hivyo ndani ya miaka hiyo sita kwake yeye ni kama ndoa na harusi yake anataka ifungwe kwenye maji.