Jumamosi , 16th Dec , 2017

Bifu kubwa linalowahusisha wakali wa mziki wa Singeli Manfongo dhidi ya Sholo Mwamba, Wasowiso na Ivan limechukua sura mpya baada ya Man Fongo kufunguka kuwa ana RB ya Wasowiso.

Manfongo amesema  anamtafuta Wasowiso ambaye amewahi kuwa meneja wake kwa madai ya kumtapeli pesa yake aliyoichukua kwa makubaliano ya kununua vifaa kwaajili ya maboresho ya gari lake lakini hakufanya hivyo na akatokomea na fedha hizo.

Akiongea na eNEWZ ya East Africa Television Manfongo amesema mkwanja aliotapeliwa na Wasowiso ni shilingi laki mbili na nusu (250,000/=).

Manfongo pia amefunguka kumshangaa Director Ivan ambaye amewahi kumlipa takribani shilingi milioni tano na akamtengenezea video ambayo haina ubora ukilinganisha na kiasi cha fedha alichotoa. “Namshanga Ivan amejiingiza kwenye bifu hilo kwani alikuwa hahusiki”, amesema Manfongo.

Manfongo alimalizia kwa kusema  anawashangaa sana wanaomsema kwamba amefulia wakati yeye ndo aliwasaidia mpaka kujulikana kwa jamii ila kwa sasa amejifunza hatarudia makosa aliyoyafanya mwanzo anajipanga upya ndani ya wiki mbili zijazo atatoa nyimbo yake mpya.