Jumatano , 30th Sep , 2015

Mgombea urais kupitia chama cha UPDP Fahmi Nasoro Dovutwa amesema hana sababu ya kufanya mikutano mikubwa ya hadhara, kwani yeye hana makosa na wala hajawaudhi wananchi, hivyo haitaji kuitumia mikutano hiyo kujisafisha.

Dovutwa ameyasema hayo alipokuwa akichat moja kwa moja na mashabiki katika kipengele cha Kikaangoni Live, kinachoendeshwa na kituo cha televisheni cha East Africa Television (EATV) na East Africa Radio, kupitia mitandao ya kijamii.

Dovutwa amesema yeye tofauti na wagombea urais wa vyama vingine, kwani wao wanatumia mikutano hiyo kujisafisha na tuhuma za kuvuruga maadili.

“mikutano ya hadhara bado sihitaji mikutano mingi kwa sababu sina makosa mengi wala sijawaudhi watu, wao wanafanya mikutano mingi ili wajitakase, wote wameshiriki kuvuruga maadili ya viongozi kwa kuweka usiri taarif za mali za viongozi”, alisema Dovutwa.

Pamoja na hayo Dovutwa amesema kwamba iwapo atafanikiwa kuwa rais wa nchi hii ataboresha nidhamu kwenye utumishi, kwani tatizo la kwanza la watanzania ni kuporwa ardhi zao, ukusanyaji wa kodi, hivyo atasimamia katika ukusanyaji wa kodi, na kusimamia mapato kupitia TRA

“Tatizo la kwanza la watanzania sio changamoto, ni matatizo ya kuporwa ardhi zao, ukusanyaji wa kodi, kodi haikusanywi nitapitia upya mfumo wa kodi, baada ya hapo mengine yatafuata kwa hiyo mimi sitapata tabu kumkamata mtu alafu nimpeleke gerezani alafu nipate tabu ya kumlisha, nitakachofanya ni kumtaka alipe kodi, tangu kuanzia alipozipata mali, na kuangalia kama amelipia kodi, hiyo itakuuwa kazi ya tra, na taasisi ya kuzuia rushwa ya wakati huo sio PCCB”, alisema Dovutwa.

KUHUSU LOWASA KUHAMIA CHADEMA

Akiongelea swala la Edward Lowassa kuhamia CHADEMA na kusisitiizia suala la mabadiliko, Dovutwa amesema Watanzania wanatakiwa wajue kuwa mabadiliko wanayoyahitaji si ya kubadilisha chama, na kuwa na viongozi wale wale wanaolalamikiwa.

“Watanzania hawawezi kudanganywa na ccm kwa kuwatoa ccm wengine kuwapeleka chadema na kusema wale ni wapinzani, wale wote ni ccm kwa hiyo mabadiliko tunaposema mabadiliko sio kubadilisha majina ya vyama, alafu ccm wale wale”, alisema Dovutwa.

Katika kuendelea kuchat na wananchi katika mtandao wakijamii,Dovutwa pia amesema ana malengo ya kulinda utamaduni wa Mtanzania ambao anaona unaporomoka kwa kuiga tamaduni za kigeni.

“Kwenye ilani yetu tumesema tutarudisha tawala za viongozi wa makabila, ambao waje kusimamia na kurudisha hadhi ya mila na desturi zetu waafrika hususani watanzania, swala la kutembea uchi sio wanawake peke yao, na wanaume, mtu anavaa bukta anatoka barazani na anaenda dukani, mtu anavaa suruali kifua nje na anakata mitaa”, alisema Dovutwa kwenye ufafanuzi wake”, alisema Dovutwa katika maelezo yake akijibu moja ya swali la mwananchi.

Pia Dovutwa amewaambia Watanzania watashangazwa na matokeo ya uchaguzi yatakapotoka, kwani sivyo ambavyo wengi wao wanayatarajia, na kuulezea uchaguzi wa mwaka huu hauna tofauti na wa miaka ya nyuma.

“Uchaguzi kama uchaguzi mwengine, hauna lolote zaidi ya hapo, kuna kushinda na kuna kushindwa basi mambo ni hayo hayo , na mjiandao kuona msichokitarajia”, alisema Dovutwa.