Alhamisi , 20th Oct , 2016

Msanii wa filamu nchini Rammy Galis amesema kwa sasa hana kabisa mahusiano ya kimapenzi na mwanadada Agness Masogange na kwamba sasa ni marafiki wa kawaida na itabaki kuwa hivyo.

Rammy Galis (Kushoto) na Agness Masogange

Galis ameyasema hayo alipokuwa akijibu maswali kutoka kwa wananchi kupitia kipindi cha KIKAANGONI kinachorushwa kupitia ukurasa wa Facebook wa EATV (eatv.tv).

“Mimi na Agnes kwa sasa ni marafiki tu wa kawaida, tumekubaliana tuishie hapo kwa sasa, na nisingependa kueleza zaidi kwa nini tumefikia uamuzi huo ila kwa sasa kila mtu ana ganga ya kwake” Amesema Galis

Katika hatua nyingine Galis amesema ana mtoto mmoja ambaye alimpata na dada mmoja wa kihindi ila familia ya dada huyo ilikataa wasioane na sasa dada huyo ameshaolewa na mtu mwingine.

Kuhusu mahusiano yake ya sasa, Galis alisema kuwa hana mpenzi na kwamba angependa kuoa lakini hajapata mwanamke wa kuoa.