Jumatatu , 19th Sep , 2016

Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu imesisitiza waajiri wote nchini kuwakata pesa kwa ajili ya kulipa deni waajiri wote waliokopeshwa na bodi hiyo.

Mkurugenzi Msaidizi wa Habari, Elimu na Mawasiliano Bwana Cosmas Mwaisobwa

Mkurugenzi Msaidizi wa Habari, Elimu na Mawasiliano Bwana Cosmas Mwaisobwa ametoa msisitizo huo wkati akijibu maswali ya wananchi kupitia ukurasa wa Facebook wa EATV, katika kipengele cha Kikaangoni,

Amesema kuwa suala hilo ni la matakwa ya kisheria hivyo hakuna muajiri yeyote anayepaswa kukwepa suala hilo, na kwamba endapo mwajiri atabainika kutokana deni hilo kutoka kwa waairiwa wake, atakumbana na mkono wa kisheria.

“Hili suala lipo kisheria, endapo mwajiri hatakata na kuwasilisha pesa hizo bodi ya mikopo anaweza kukumbana na faini, au hatua zaidi ikiwa ni pamoja na kufikishwa mahakamani” Alisema Mwaisobwa .

Aliongeza kuwa ili kuwabana waajiri wanaokwepa kukata madeni hayo, serikali kuanzia mwaka ujao wa fedha imeagiza wakaguzi wa mahesabu akiwemo Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) kutopitisha hesabu za kampuni au taasisi yoyote ambazo hazitaonesha kukatwa kwa deni hilo.

“Kuanzia sasa ili hesabu zipitishwe, ni lazima tuone jinsi ambavyo madeni hayo yamekatwa, vinginevyo kampuni au taasisi inapata hati chafu, jambo ambalo lina madhara makubwa, kwahiyo ni bora waajiri wakajiepusha na mambo kama hayo”.

Alisema kiwango kinachopaswa kukatwa ni asilimia 8 ya mshahara wa mfanyakazi ambaye alikopshwa na bodi hiyo.

Mwaisobwa pia alionya waajiri wanaokata madeni hayo bila kuyawasilisha bodi ya mikopo, na kusema kuwa endapo watabainika watachukuliwa hatua za kisheria.

Kuhusu malalamiko ya baadhi ya watu kuandikiwa deni kubwa kuliko pesa waliyokopa, Mwaisobwa amesema kila mtu atalipa pesa ileile aliyokopeshwa, pamoja na asilimia 6 ambayo ni kiwango cha kulinda thamani ya fedha Value Retantion Fee), na endapo amechelewa kulipa, atatakiwa kulipa na fain ambayo ni asilimia 10 ya fedha aliyokopshwa wa mwaka.

Hadi sasa bodi hiyo imekwishakopesha kiasi cha takribani trilioni 2.44.

Fuatilia Kikaangoni kila Jumatano, saa 8:00 mchana.