Jumamosi , 28th Sep , 2019

Muandaaji wa mashindano ya ulimbwende ya Miss Tanzania, Basilla Mwanukuzi amesema kuwa hajawahi kukutana na malalamiko yoyote katika mitandao ya kijamii yanayomlalamikia kuwa ni mtu asiyekubali kupokea ushauri.

Basilla Mwanukuzi

Akizungumza na EATV & EA Radio Digital leo Septemba 28, 2019, Basilla amesema kuwa yeye haoni kama upo umuhimu wa watu kuendelea kulalamika kwenye mitandao ya kijamii na kwamba ni vigumu kumjibu kila mtu anayeandikia kwenye mtandao.

''Suala la watu kunilalamikia sijawahi kukutana nalo, ni jipya kabisa halafu kwanini watu wanapenda kulalamika na wanaoshauri sijui wanashauri nini mitandaoni. Unakutana na mtu hata akaunti yake haijulikani, bora hata angekuwa 'verified' unajua huyu ni mtu gani'', amesema Mwanukuzi.

Akimzungumzia mshindi wa Miss Tanzania 2019, Sylvia Sebastian, Mwanukuzi amewaomba watanzania kuendelea kutembelea mitandao yake ya kijamii na ku 'like' picha zake  ili aweze kufanikisha kunyakua taji la urembo wa dunia , mashindano ambayo yanatarajiwa  kufanyika nchini Uingereza.