Jumanne , 30th Mar , 2021

Kocha msaidzi wa KMC ya Kinondoni Habibu Kondo amekiri timu yake kwa sasa hawapo tena kwenye kinyang'anyiro cha ubingwa zaidi ya kuangalia nafasi nne za juu na kujikita zaidi kwenye kombe la shirikisho la Azam.

Kocha wa KMC Habibu Kondo

Kondo aliyasema hayo leo tarehe 30/03/2021 alipokuwa anahojiwa na Eatv saa 1 mara baada ya timu yake kuanza rasmi mazoezi mahususi kwa ajili ya kumalizia ligi ambayo imebakiza mechi 11 kwa timu zilizocheza michezo mingi zaidi .

Kocha Habibu Kondo alisema '' awali ya yote wakati ligi inaanza tulikuwa na imani ya kutwaa ubingwa msimu huu, lakini kadri muda unavyokwenda imani yetu inatoweka kutokana na matokeo mabaya yetu tuliyoyapata kabla ya ligi kusimama''

''Kwa sasa akili zetu tumeziwekeza zaidi katika michuano ya kombe la shirikisho ambapo tutakutana na Dodoma jiji katika hatua hii ya robo fainali, ambapo pia ni njia ya mkato kupata uwakilishi wa kimataifa'' aliongeza Kondo

KMC ipo kwenye nafasi ya 7 kwenye msimamo wa ligi ikiwa na alama 32 baada ya kushuka dimbani mara 23 huku Yanga akiongoza msimamo huo wakiwa na alama 50 kwenye michezo 23,wakifuatiwa na Simba yenye alama 46 katika michezo 20 waliokwisha kucheza , Azam,Biashara, Ruvu na Dodoma jiji zikifuatana juu yao.