Alhamisi , 30th Jun , 2016

Kocha wa Real Madrid Zinedine Zidane anamtaka kiungo mkabaji wa Leicester City na Ufaransa aliye kwenye kiwango bora kwa sasa aking'ara katika michuano ya Euro 2016, N'Golo Kante pia amemvutia kocha wa Manchester United Jose Mourinho.

Kiungo wa Leicester City Mfaransa N'Golo Kante.

Kocha wa mabingwa wa soka wa klabu bingwa barani Ulaya Real Madrid Mfaransa Zinedine Zidane ametamka wazi kuwa sasa ameridhika na kiwango bora cha kiungo fundi wa klabu ya Leicester City ambaye kwa sasa anafanya vema na timu ya taifa ya Ufaransa iliyo katika michuano ya mataifa ya Ulaya mwaka 2016 inayoendelea nchini Ufaransa ikiwa tayari imeshaingia katika hauta ya 8 bora.

N'Golo Kante katika mkataba wake na Leicester City unamruhusu kuondoka kwa mabingwa hao wa EPL kwa kitita cha pauni milioni 20 kutokana na dau hilo hii ni baada ya kiungo huyo mkabaji kuwa katika kiwango bora kwa sasa nakuonekana dhahabu na hivyo kuzivutia klabu nyingi kubwa barani Ulaya kama Manchster United, Arsenal na sasa Real Madrid nayo imemwingiza kati rada zake.

Zidane ambaye enzi za uchezaji wake alikuwa kiungo fundi wa ushambuliaji akimudu kucheza kwa ufundi na mbinu nyingi na utaalamu wa mipira iliyokufa[ free kick] ameonekana kupania zaidi kupata saini ya kiungo huyo mfupi mwenye asili ya Afrika ili kuimarisha kikosi chake katika eneo la safu kiungo baada ya kuwa akimtegemea kiungo mkabaji mmoja pekee Casemiro.

Zidane kwa muda mrefu sasa tangu mwezi Januari mwaka huu amekuwa akimfuatailia kiungo huyo mfupi mwenye nguvu, kasi na fundi wa pasi za mwisho na kupandisha mashambulizi na sasa ameonyesha kukoshwa na uwezo wake na ameamua kuwataka mabosi wa timu yake kuhakikisha wanamwaga fedha ili kuharakisha dili la kumnasa kiungo huyo linakamilika kabla halijaingiliwa na timu nyingine ambazo nazo zimeonyesha nia yakutaka huduma yake.

Kante mwenye miaka 25 alinunuliwa na Leicester City katika dirisha kubwa la usajili majira ya joto msimu uliopita akitokea timu ya Canes ya Ufaransa kwa Ada ya pauni milioni 6 na tangu hapo ametokea na kuibuka kuwa mmoja wa viungo bora kabisa na amekuwa mchezaji tegemeo kwa klabu yake na sasa nchi yake ambayo inamajukumu ya kimataifa kwa sasa katika michuano ya Euro 2016 ambapo Ufaransa ikiwa chini ya kocha Didier Deschamps imetinga hatua ya robo fainali ikitaraji kucheza na Iceland siku ya Jumapili Julai 3 mwaka huu.