Jumatano , 21st Feb , 2018

Shirikisho la soka Barani Afrika limeithibitishia Simba SC tarehe rasmi ya michezo yao miwili ya Kombe la Shirikisho dhidi ya Al Masry ya Misri, ambapo mechi ya kwanza itapigwa Dar es salaam na kisha Simba kwenda Misri kwa marudiano.

Taarifa ya CAF kwa vilabu vilivyofuzu kutoka raundi ya awali imeonesha Simba itakuwa dimbani Machi 6 kucheza na wageni wao Al Masry kabla ya Simba kusafiri Machi 16 kwenda mjini Port Said Misri kwenye mchezo wa marudiano.

Kwa upande wa klabu ya Simba kupitia kwa msemaji wake Haji Manara amesema wao wameipokea ratiba hiyo bila shida na imewafurahisha kwasababu wataanzia nyumbani hivyo watatumia vizuri nafasi hiyo na kushinda mchezo ili kurahisisha kazi nchini Misri.

Simba imevuka hatua ya awali baada kuifunga Gendarmerie ya Djibouti kwa jumla ya mabao 5-0 katika mechi mbili ambapo jijini Dar es salaam Simba ilishinda 4-0 na ugenini jana kushinda 1-0.