Jumatano , 19th Sep , 2018

Gumzo kubwa katika mchezo wa jana wa Liverpool na PSG ni katika staili ya ushangiliaji ya mshambuliaji wa Liverpool, Roberto Firmino baada ya kufunga bao la tatu na la ushindi katika dakika za majeruhi.

Pichani, mshambuliaji wa Liverpool, Roberto Firmino (kushoto) na mshambuliaji wa klabu ya Simba, Meddie Kagere.

Firmino alishangilia kwa staili ya kuziba jicho moja, staili ambayo kwa mashabiki wa soka nchini Tanzania na hata Afrika Mashariki wanaishuhudia kwa mshambuliaji wa klabu ya Simba, Meddie Kagere ambaye anashangilia kwa staili ya kuziba jicho moja kila anapofunga bao.

Kagere amekuwa akiitumia staili hiyo tangu akiwa katika klabu ya Gor Mahia ya Kenya na hata anapofunga bao katika timu yake ya taifa ya Rwanda.

Mashabiki na wadau wa soka wamekuwa wakikinzana juu ya nani mwanzilishi wa staili hiyo au nani ambaye ameipa umaarufu kiasi cha kujukikana kwa kiasi hicho. Wapo wanaosema kuwa Kagere ndiye anastahili kuitwa mwanzilishi wa staili hiyo au aliyeipa umaarufu huku wengine wakisema kuwa mshambuliaji huyo wa Simba ameiga staili hiyo kutoka Ulaya ambako wachezaji wengi wamekuwa wakiitumia na hastahili kuwa ndiye mchezaji aliyeipa umaarufu.

Kwa upande wa Roberto Firmino, yeye amekuwa ni mchezaji mwenye staili nyingi za ushangiliaji, misimu miwili iliyopita aliwahi kuwa na staili maarufu ya ushangiliaji ya kuvua shati anapofunga kabla ya kuiacha kutokana na kuadhibiwa kwa kadi za njano mara nyingi alipokuwa akifanya hivyo.

Pia aliwahi kuwa na staili maarufu ya ushangiliaji ya ‘Samba dance’ aliokuwa akicheza na Mbrazil mwenzake Phillipe Coutinho aliyetimkia Barcelona. Staili hizo  zimekuwa zikitumiwa na wachezaji wengi wa Brazil ambazo zinatokana na ngoma maarufu nchini kwao ya ‘Samba’.

Mwisho wa siku ukweli haujajulikani kuwa ni nani hasa mwanzilishi au mchezaji aliyeipa umaarufu staili hiyo kiasi cha kummilikisha kuwa ni yake kama ilivyo staili maarufu ya ushangiliaji ya Cristiano Ronaldo, ambayo aliitumia pia katika bao lake la kwanza kwenye mchezo wa Serie A wikiendi iliyopita dhidi ya Sassuolo.