Jumatatu , 20th Oct , 2014

Wanamichezo wa mchezo wa sanaa za mapigano mtindo wa Goju Kai Karate toka vyama vya mchezo huo kwa nchi tatu za Afrika mashariki wamekutana jijini Dar es salaam katika tamasha maalumu la mafunzo na maonesho ya mitindo ya mchezo huo.

Baadhi ya washirkiki wa semina na onyesho la mchezo wa karate mtindo wa Goju Kai katika picha ya pamoja.

Vyama vya mchezo wa sanaa za mapigano Karate mtindo wa Goju Kai kutoka nchi za Kenya, Uganda na wenyeji Tanzania wameungana na kuunda umoja wa vyama hivyo kwa nchi hizo ambavyo vilikutana jijini Dar es salaam katika semina maalumu iliyoongozwa na Rais wa Goju Kai Afrika Peter Brandon.

Rais wa chama cha Goju Kai Tanzania ambaye ni Rais wa shirikisho la karate nchini TKF Sensei Geofrey Kalonga amesema wazo la kuunda umoja huo ni kuanzisha ushirikiano baina ya nchi hizo katika kukuza sanaa hiyo hasa kupitia mashindano ya pamoja.

Naye Rais wa Goju Kai Afrika Peter Brandon ambaye alikuwa mgeni rasmi katika semina na mashindano maalumu ya kuonesha aina mbalimbali za mitindo ya Goju Kai onesho lililofanyika katika uwanja wa ndani wa taifa amepongeza mpango huo hasa ukiwa na mtazamo wa kukuza sanaa hiyo kwa vijana wadogo.

Pia aliwataka wanamichezo hao kucheza kwa kujifunza na si kukamiana na kila mtu amweshimu mwenzake na wajenge ushirikiano ambao utasaidia kuinua viwango vyao na mchezo kwa ujumla.