Jumatatu , 21st Aug , 2017

Kocha wa timu ya TMT, Evans Davies Mwaseba amefunguka na kudai sababu iliyopelekea mpaka timu yake kufungwa katika 'game 3' kwa pointi 87-82 ni kutokana na wachezaji wake kuhamaki baada ya kuchezewa faulu sana na wapinzani wao.

Kocha wa timu ya TMT, Evans Davies Mwaseba.

Mwaseba ameeleza hayo baada ya timu yake kuonekana kuzidiwa katika robo ya nne ya mchezo wa fainali uliyochezwa katika viunga vya Don Bosco Oysterbay Jijini Dar es Salaam na kusababisha kuwaruhusu wapinzani wao waendelea kupachika mpira katika goli lao.

"Kilichosababisha tufungwe katika 'game 3' na Mchenga BBall Stars ni kutokana sisi kuhamaki kuanzia kwenye benchi la wachezaji mpaka wale waliyokuwa ndani wakicheza baada ya kuona wakichezewa faulo nyingi, lakini tunaenda kujipanga vizuri kuelekea mechi ijayo ya game 4 ili tuweze kufanya mashabulizi vizuri na tuweze kuziba mapungufu yaliyoweza kujitokeza katika mechi iliyopita", alisema Mwaseba.

Pamoja na hayo, TMT mpaka sasa imeweza kushinda mechi 1 na kufungwa 2 katika fainali hizi zinazoendelea huku mpinzani wake Mchenga BBall Stars akiwa ameshinda mechi 2 na kupoteza mechi 1.

Mshindi wa kwanza katika fainali za Sprite BBall Kings anatarajiwa kuondoka na kitita cha Milioni 10 huku mshindi wa pili kuondoka na Milioni 3 na kumaliziwa na mchezaji bora 'MVP' kupata Milioni 2.