Jumatatu , 4th Feb , 2019

Mwekezaji mkuu wa klabu ya Simba Mfanyabiashara, Mohemmed Dewji amesema hajakata tamaa na matokeo ya Simba japo yanamuuma sana.

Wachezaji wa Simba na mwekezaji Mo Dewji

Baada ya kuwa kimya kwa muda mrefu tangu Simba ilipofungwa na AS Vita na pia kufungwa na Al Ahly Jumamosi iliyopita Mo Dewji, amemua kuweka wazi maumivu yake.

''Roho yangu bado inaniuma. Naipenda sana Simba, na bado sijakata tamaa. Roma haikujengwa kwa siku moja'', ameandika Mo Dewji kwenye mtandao wa Twitter.

Simba ambayo imerejea nchini mchana wa leo ikitokea Misri ambako ilicheza mchezo wa tatu wa kundi D dhidi ya Al Ahly na kufungwa mabao 5-0, ipo kwenye nafasi ya tatu ya kundi D ikiwa na alama 3.

Simba bado ina mechi mbili za nyumbani dhidi ya AS Vita na Al Ahly na mechi moja ugenini dhidi ya JS Saoura ya Algeria.

Kundi D linaongozwa na Al Ahly yenye alama 7 ikifuatiwa na AS Vita Club yenye alama 4 huku Simba wakiwa nafasi ya tatu na alama 3 na JS Saoura wakishika mkia na alama 2.