Ijumaa , 7th Jun , 2019

Kikosi cha Timu ya Taifa ya Tanzania, Taifa Stars kinategemewa kusafiri leo kuelekea nchini Misri ambako itaweka kambi ya mwisho kwa ajili ya kujiandaa na michuano ya AFCON itakayoanza mwishoni mwa mwezi huu.

Mazoezi ya Taifa Stars

Stars inasafiri na nyota 32 huku Nyota 7 wakiachwa, ambapo miongoni mwa walioachwa ni Jonas Mkude, Ibrahim Ajib, Ayoub Lyanga, Ally Ally, Kassim Khamis, Kennedy Wilson na Shomari Kapombe.

Kocha Amunike amesema kigezo kilichotumika kuwaacha nyota hao ni viwango vyao mazoezini na nidhamu huku akisisitiza kuwa anajua watu wana matamanio yao juu ya wachezaji fulani lakini nidhamu na utimamu wa viwango vyao katika mazoezi ndiyo kipaumbele kikubwa mbali ya Kapombe ambaye bado hajawa fiti.

Aidha Amunike amesema amewajumuisha makinda Kelvin John na Boniphace ili kuwapa uzoefu zaidi akitambua umuhimu wa kuimarisha vijana kwa soka la baadae.

Stars pia inategemea kucheza mechi mbili za kirafiki nchini Misri, mechi ya kwanza dhidi ya wenyeji Misri, Juni 13 na mechi nyingine dhidi ya Zimbabwe mnamo Juni 16 kabla ya kuanza kwa michuano hiyo.