Jumatano , 25th Mar , 2020

Afisa Habari wa klabu ya Simba, Haji Manara ameeleza kukoshwa na kazi ya kiungo mkabaji wa klabu ya Yanga, Papy Tshishimbi na kusema kuwa hata yeye anapenda kumuona mchezaji huyo Msimbazi.

Haji Manara na Papy Tshishimbi

Hivi karibuni zimesambaa taarifa mbalimbali katika mitandao ya kijamii kwamba kiungo huyo yupo njiani kuondoka katika klabu ya Yanga, huku mkataba wake ukiwa ukingoni kumalizika msimu huu.

Kupitia ukurasawake wa Instagram, Haji Manara amesema kuwa yeye ni shabiki mkubwa wa mchezaji huyo na anapenda kumuona siku moja akiichezea Simba.

"Box to box midfielder' Papy Tshishimbi, siyo siri mimi ninamshabikia sana. Nikiulizwa natamani siku moja aje kucheza Simba, Yes napenda iwe hivyo ila kwa sasa bado ni mchezaji wa Gongowazi, lakini huwezi kujua ya kesho", amesema Manara.

Mchezaji mwenyewe Tshishimbi amesema kuwa yuko tayari kufanya kazi na klabu yoyote ambayo itafikia makubaliano naye. Mpaka sasa imebakia miezi takribani minne mkataba wa mchezaji huyo kumalizika katika klabu ya Yanga.