Ijumaa , 15th Jun , 2018

Msanii wa mziki wa Bongo Fleva ambaye pia ni shabiki na mchezaji wa mpira wa Kikapu Mh.Temba, amefunguka kuwa thamani ya mchezo huo nchini, imeanza kuwa  kubwa kwakuwa wadhamini wa mchezo huo wameanza kujitokeza kwa wingi kama ilivyo kwenye michezo mingine.

Akizungumza na www.eatv.tv  leo Temba amesema kazi kubwa  ni kupata fursa kwahiyo fursa imepatikana kwahiyo watu watumie wadhamini hao kufika mbali katika kuitangaza nchini na wao wanufaike kupitia mchezo huo.

Temba amesema sasa ivi wadhamini wanaandaa mashindano na kuwapa hamasa watu kwa kutoa zawadi  na hiyo inafanya watu kucheza kwa nguvu na kuwekeza ndoto zao kwenye kikapu kwa wingi.

"Hii inasaidia, kuona wadhamini wanajitokeza kwa wingi ni jambo zuri, kwa kuanza  kuandaa mashindano, pia kuwapa  zawadi washindi  pia  MVP, kupewa pesa ambazo mwisho wa siku zinawasaidia kuendeleza maisha yao na vipaji vyao kwahiyo sasa ivi mchezo naona unakuwa mzuri na mkubwa pia ,"amesema Temba.

Pia ameongeza kwa kusema zamani  kulikuwa hakuna wadhamini wa kutoa pesa za kuendeleza mchezo huo, lakini sasa hivi mchezo wa kikapu unaonekana kuwa ajira kama ambayo michezo mingine ilivyo ajira.

Mbali na Temba, mshindi wa 'Most valuable player' kutoka mashindano ya Sprite BBall Kings 2017 Rwehabura Munyagi,  'Barongo' amesema  mchezo wa kikapu sasa hivi unafanya watu kuishi vizuri na watu wanaelewa kuhusu mchezo huo.

"Elimu kuhusu kikapu sasa hivi naona inatolewa kuanzia mashuleni na watu wanakuwa wakiwa wanaona mpira wa kikapu unawalipa watu, mpaka sasa nina miaka 40 lakini enzi mimi nakuwa kulikuwa hamna hamasa ya mchezo huo lakini sasa ivi serikali naona inaweka nguvu  kwenye mchezo wa kikapu hiyo maana yake nikuwa kikapu kimekuwa ajira,"amesema Barongo.

Hata hivyo East Africa Television Limited ikishirikiana na kinywaji baridi cha Sprite  kwakuona umhimu wa mchezo huo imekuwa ikiandaa mashindano ya Sprite Bball Kings na kwa mwaka huu mashindano yamezinduliwa ambapo usaili unaanza kesho Juni 16, 2018 na utafanyika Mlimani City Mall.