Jumatatu , 11th Dec , 2017

Kocha wa Manchester United Jose Mourinho, amesema huenda mbio za ubingwa wa EPL zikawa zimefika tamati baada ya timu yake kupoteza 2-1 dhidi ya mahasimu wao Manchester City jana usiku.

Akiongea na wanahabari baada ya mchezo Mourinho amekiri kuwa ni vigumu kuikamata Manchester City ambayo hivi sasa imewaacha kwa tofauti ya pointi 11. “Mbio zinaweza kuwa zimefika tamati kutokana na tofauti ya alama iliyopo sasa”, amesema Mourinho.

Mourinho ameongeza kuwa kikosi cha Man City ni bora lakini pia kinasaidiwa na bahati ndio maana ni vigumu kuwapata. "Manchester City ni timu nzuri sana na imekuwa na bahati sana na ni vitu ambavyo vinatokea kwenye soka, lakini tutapigana na kujaribu kupunguza fotauti ya alama”, ameongeza Mourinho.

Mabao ya David Silva na Nicolas Otamendi yalitosha kuimaliza Manchester United kwenye uwanja wake wa Old Traford ambapo ilikuwa haijapoteza mechi 40 tangu Septemba 2016 ilipofungwa na Man City.

Baada ya mchezo wa jana Manchester City sasa imeweka rekodi ya kushinda mechi 14 mfululizo za ligi ndani ya msimu mmoja wa EPL.