Ijumaa , 23rd Feb , 2018

Timu ya Mtibwa Sugar imejiwekea malengo ya kutwaa ubingwa wa kombe la shirikisho nchini ili kurudisha heshima ya klabu hiyo ambayo iliwahi kutwaa ubingwa wa ligi kuu soka Tanzania Bara.

Hayo yameelezwa na kocha wa Mtibwa Sugar, Zuberi Katwila ambaye amesema  wanataka kurudi kwenye michuano ya Afrika na katika kuhakikisha wanatimiza hilo lazima waibuke mabingwa wa Kombe la Shirikisho FA.

Akiongelea mchezo wao wa 16 bora dhidi ya Buseresere FC Katwila amesema wanatarajia kupata ushindani mkali kutoka kwa mabingwa hao wa mkoa wa Geita ambao wanacheza ligi daraja la Pili. Buseresere FC imetinga hatua hiyo baada ya kuitoa timu ya Kagera Sugar inayoshiriki ligi daraja la kwanza.

Tayari timu za zote zilizocheza fainali ya FA Mei 27, mwaka jana kwenye Uwanja wa Jamhuri mjini Dodoma ambzo ni Simba SC walioifunga Mbao FC, zimeshatolewa kwenye michuano hiyo kabla ya hatua ya Robo Fainali.

Mchezo kati ya timu hizo mbili unatarajiwa kuchezwa kesho kwenye uwanja wa Nyamagana jijini Mwanza. Mtibwa Sugar kwasasa inashika nafasi ya sita kwenye msimamo wa ligi kuu ikiwa na alama 27.