Ijumaa , 18th Aug , 2017

Nahodha wa timu ya TMT, Isihaka Masoud ameomba radhi kwa utovu wa nidhamu aliyoonyesha katika mechi ya 'game 1' ya fainali za Sprite BBall Kings na kudai kilichotokea siku hiyo hakikuwa dhumuni lake ila hasira ndizo zilizomponza.

Nahodha wa timu ya TMT, Isihaka Masoud.

Isihaka amesema hayo leo baada ya kupita siku chache tokea alipofanya kitendo cha utovu wa nidhamu kwa kuwa tuhumu waamuzi 'Official' wa mchezo kuwa wanawabeba timu ya Mchenga BBall Stars kwa kuwa wao walifungwa kwa pointi 101-71 wakati alipokuwa akifanyiwa mahojiano 'Live' kupitia EATV uwanjani hapo jambo ambalo ni kinyume na sheria na taratibu za mchezo huo.

"Nimejisikia vibaya mwenyewe kwa kitendo nilichokifanya siku hiyo mpaka nafika nyumbani, nikawa najiuliza ni mimi kweli nimeongea yale maneno je watu watanifikiliaje?. Lakini naomba msamaha kwa washabiki wangu wote wa TMT, uongozi wa EATV, East Africa Radio, kwa mdhamini wa mashindano haya Sprite, TBF pamoja na watu wote wanaopenda mpira wa kikapu", alisema Isihaka.

Pamoja na hayo, Isihaka amesema kwa sasa amejifunza ni wapi anapaswa apeleke malalamiko yake pindi yanapotokea awapo uwanjani.

TMT inatarajiwa kushuka dimbani kesho kuvaana na Mchenga BBall Stars katika mchezo wa tatu wa fainali za Sprite BBall Kings katika viwanja vya Don Bosco Oysterbay Jijini Dar es Salaam majira ya saa tisa mchana kwa saa za Afrika Mashariki na Kati.

Msikilize hapa chini Nahodha wa TMT, Isihaka Masoud anavyoendelea kuongea zaidi.