Jumatatu , 15th Dec , 2025

BEKI wa kati wa Liverpool na timu ya taifa ya Ufaransa, Ibrahima Konate, 26, rasmi ameiingiza vitani Paris Saint-Germain ambayo imeonyesha nia ya kutaka kumsajili katika dirisha lijalo la majira ya baridi na kuipiku Real Madrid.

Ibrahima Konate

Konate amekuwa nguzo muhimu katika safu ya ulinzi ya Liverpool kwa muda sasa lakini anadaiwa kutaka kuondoka mwisho wa msimu huu mkataba wake utakapomalizika.

Awali, staa huyu alitajwa kuwa na asilimia kubwa za kwenda Madrid, lakini sasa mambo yanaonekana kubadilika baada ya PSG pia kuonyesha nia ya kutaka kumsajili.

Konate amekataa kusaini mkataba mpya wa kuendelea kusalia Liverpool licha ya kufanyika kwa majadiliano ya mara kwa mara kati ya wawakilishi wake na mabosi wa Liverpool.

Liverpool inaonekana kuwa tayari kumuuza katika dirisha lijalo badala ya kusubiri kuona akiondoka bure mwisho wa msimu huu.

Tangu kuanza kwa msimu huu Konate amecheza mechi 23 za michuano yote na kufunga bao moja.

Hata hivyo, wakosoaji wamekuwa wakimshambulia Konate kuwa amechangia matokeo ya kusuasua ya Liverpool kwa msimu huu.