Jumatatu , 19th Mar , 2018

Nyota wa Real Madrid Cristiano Ronaldo amemfunika nyota wa Barcelona Lionel Messi pamoja na washambuliaji wengine akiwa ndiye mchezaji aliyefunga mabao mengi zaidi ndani ya mwaka 2018.

Ronaldo amefanikiwa kufikisha mabao 21 kwenye mashindano yote tangu mwaka 2018 uanze, baada ya jana usiku kufunga mabao 4 kwenye ushindi wa mabao 6-3 iliyopata Real Madrid dhidi ya Girona.

Kwa idadi hiyo ya mabao imemfanya nyota huyo raia wa Ureno kuwazidi nyota kadhaa akiwemo mpinzani wake Lionel Messi mwenye mabao 16 pekee ndani ya mwaka 2018 katika michuano yote.

Kwa upande mwingine Ronaldo amefanikiwa kufunga Hat-trick yake ya 50 katika maisha yake ya soka. Kati ya hizo 44 ameifungia Madrid, 5 timu ya taifa ya Ureno na 1 Manchester United.

Mbio za kiatu cha dhahabu kwa La Liga maarufu (PICHICHI) zinaongozwa na Messi mwenye mabao 25 akifuatiwa na Ronaldo mwenye mabao 22. Mbio za Ubingwa zinaongozwa na Barcelona wenye alama 75 wakifuatiwa na Atletico Madrid wenye alama 64.