Jumanne , 18th Dec , 2018

Shirikisho la Soka Tanzania TFF limetangaza kuwa Timu ya Taifa ya Vijana ya Tanzania U17 “Serengeti Boys” itashiriki kwenye mashindano maalumu ya maandalizi ya Afcon U17 yatakayofanyika Antalya nchini Uturuki mapema mwakani.

Kikosi cha Serengeti Boys

Kwa mujibu wa taarifa ya TFF kupitia tovuti yake, mashindano hayo yameandaliwa na Shirikisho la Soka barani  Afrika CAF kwa ushirikiano na Shirikisho la Soka barani Ulaya UEFA, ambapo yanatarajia kuanza Februari 22,2019 mpaka Machi 2,2019 na kushirikisha jumla ya timu 12 kutoka Afrika na Ulaya.

Mbali na Serengeti Boys, nchi nyingine za Afrika zitakazoshiriki katika mashindano hayo ni pamoja na Angola, Morocco, Cameroon, Uganda, Nigeria, Senegal na Guinea ambazo zitaungana na timu nne kutoka bara la Ulaya.

Serengeti Boys imewasili nchini jana Desemba 17 ikitokea nchini Botswana ambako ilialikwa kushiriki mashindano ya mataifa ya kusini mwa Afrika kwa vijana chini ya miaka 17, ambako imefanikiwa kurudi na ubingwa wa michuano hiyo baada ya kuifunga Angola kwa mikwaju ya penalti 6-5 katika mchezo wa fainali.