Alhamisi , 20th Dec , 2018

Baada ya kilio cha muda mrefu cha Rais John Magufuli juu ya timu za Tanzania kutochukua ubingwa katika michuano mbalimbali ya kimataifa, hatimaye Rais amekiri kufutwa chozi na ubingwa wa COSAFA walioupata vijana wa Serengeti Boys.

Rais John Magufuli

Akieleza furaha ya Rais Magufuli mbele ya vijana wa Serengeti Boys leo kwenye hafla ya chakula cha pamoja iliyoandaliwa na mlezi wa timu hiyo ambaye ni Mwenyekiti Mtendaji wa Makampuni ya IPP Dkt. Reginald Mengi,  Mwakyembe amesema Rais amefurahia sana ubingwa huo.

''Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mh. John Pombe Magufuli amefurahi sana kwa ushindi wenu na amewapongeza sana kwa kuiwakilisha vyema nchi, salamu zenu nitazifikisha leo nitamwambia Vijana wako wamekuletea zawadi ya Christmas'', amesema Mwakyembe.

Serengeti Boys

Aidha Mwakyembe ameongeza kuwa walichokifanya Serengeti Boys, kuchukua Kombe la Kanda ya COSAFA ni jambo kubwa na limepokewa vyema na kila mtanzania hivyo waendelee kujipanga kwaajili ya michuano ya AFCON 2019 itakayofanyika hapa nchini.

Serengeti Boys walitwaa ubingwa huo Jumapili ya Desemba 16, 2018 kwa kuwafunga Angola kwa Penati 6-5 baada ya kutoka sare ya bao 1-1 katika dakika 90 za kawaida.