Jumatano , 18th Aug , 2021

'Sports Countdown' ya East Africa radio inakuhesabia zile stori sita kali za kimichezo leo Agosti 18, 2021 kupitia 'Spa Breakfast' saa moja na robo kila Jumatatu hadi Ijuamaa. Gumzo ni Ronaldo kukanusha kuihama Juventus.

Nyota wa Juventus, Cristiano Ronaldo 'ÇR7' akishangilia baada ya kufunga moja ya bao kwenye mchezo wa Ligi kuu ya Italia msimu uliomalizika.

6 - Ni idadi ya mashuti yaliyolenga lango kwa kila timu kwenye fainali ya ngao ya hisani ya jamii nchini Ujerumani 'DFL Super Cup' kati ya Borussia Dortmund na Bayern Munich iliyochezwa usiku wa kuamkia leo.

Mchezo huo umemalizika kwa Bayern Munich kupata ushindi wa mabao 3-1 dhidi ya Dortmund na kutwaa kombe hilo kwa mara ya saba na kuendelea kuwa bingwa wa kihistoria.
Mabao ya Bayern Yamefungwa na Robert Lewandoski aliyefunga mabao mawili, Thomas Muller akifunga moja huku Marco Reus akifunga bao la kufutia machozi kwa upande wa Dortmund.

5 - Ni idadi ya wachezaji waliosajiliwa na klabu ya Simba mpaka hivi kwenye dirisha kubwa la usajili.

Idadi hiyo imetimia baada ya hapo jana kuthibitisha kumsajili kiungo Abdulsamad Ally Kassim kutoka visiwani Zanzibar kwa kandarasi inayoelezwa na miaka miwili akiwa mchezaji huru baada ya kutemwa na Kagera Sukari. Wachezaji wengine waliosajiliwa rasmi na Simba ni, Yusuph Mhilu ambaye usajili wake una utata baada ya khatibu wa Kagera Ali Masoud kudai bado mchezaji huyo anamkataba wa mwaka mmoja na Kagera, Mzawa Israel Patrick Mwenda, Henock Inonga Baka, Pape Ousmane Sakho, Peter Banda na Duncan Nyoni.

4 - Ni idadi ya timu zinazounda kila kundi katika makundi 6 ya kuwania nafasi ya kufuzu AFCON kwa msimu ujao.

Kundi A - Cameroon, Burkina Faso, Ethiopia na Cape Verde.

Kundi B - Senegal, Zimbabwe, Guinea na Malawi

Kundi C - Morocco, Ghana, Comoro na Gabon.

Kundi D - Nigeria, Egypt, Sudan na Guinea Bissau.

Kundi E - Algeria, Sierra-Lione, Equatorial Guinea na Ivory Coast.

Kundi F - Tunisia, Mali, Mauritania na Gambia.

3 - Ni idadi ya miaka iliyopita tokea nyota wa timu ya taifa ya Ureno, CR7 ajiunge na klabu ya Juventus 'kibibi kizee cha Turin' akitokea Real Madrid kwa ada ya uhamisho ya paundi milioni 100 za England na mpaka hivi sasa amefanikiwa kufunga mabao 101 kwenye michezo 133 aliyoichezea timu hiyo.

Nyota huyo ambaye ni mkali wa kufumania nyavu amevunja ukimya baada ya uvumi wa kuihama klabu hiyo na kushika kasi na kuhusishwa na Real Madrid, Man City na PSG. Ronaldo amesema watu wanatumia jina lake vibaya kuongea watakavyo jambo ambalo amesema ni kumkosea heshima yeye na hata timu anazohusishwa nazo na kukazia kuwa bado yupo Juventus kwa sasa.

2 - Ni idadi ya siku zilizopita tokea mcheza kikapu Patrick Beverley ajiunge na Memphis Glizzles akitokea timu ya Los Angeles Clippers kama sehemu ya mabadilishano ya wachezaji watatu ili kuwezesha usajili wa Eric Bledsoe kutoka Memphis kwenda Clippers.

Nyota huyo mwenye umri wa miaka 33 kwasasa amefanyiwa uhamisho mwengine kwani timu yake ya sasa Memphis Glizzles imempeleka Minnesota Timberwolves kwa kubadilishana na wachezaji wawili wa Timberwolves, Jarret Culver na Juancho Hernangomez.

1 - Ni nafasi ya ubora anayoshikilia Johanna Konta kwenye viwango vya ubora vya wacheza tennisi nchini England na wa 41 duniani kwa upande wa wanawake. 

Mwanadada huyo ameendelea kuwa na msimu mbaya baada ya usiku wa kuamkia leo kutolewa kwenye mzunguko wa kwanza wa mashindano ya Cincinnati Open inayofanyika nchini Marekani kwa kufungwa seti 3-6, 7-6 & 6-2 na Karolina Muchova raia wa Czech mwenye umri wa miaka 24 anayeshika nafasi ya 23 kwa ubora duniani.

Kwa ushindi huo, Muchova atacheza na mshindi wa zamani wa michuano ya US Open, Mwanamama Bianca Andreescu kwenye mzunguko wa pili wa mashindano hayo ya kujiandaa na US Open itakayoanza Agosti 30 mwaka huu.