Jumamosi , 17th Mei , 2014

Baada ya uongozi wa manispaa ya jiji la Dar es salaa, kusuasua kutoa majibu ya ombi la klabu ya Yanga kutaka kuongezewa eneo kidogo la kufanya ujenzi wa kitega uchumi, wazee wa timu hiyo wajipanga kwenda kwa mkuu wa mkoa

Baadhi ya viongozi wa Baraza la Wazee wa Yanga

Sakata la ujenzi wa kitega uchumi cha klabu ya soka ya Yanga limechukua sura mpya mara baada ya Baraza la wazee wa klabu hiyo kuamua kwa kauli moja kwenda ofisi ya mkuu wa mkoa wa Dar es salaam kufikisha kilio chao juu ya ombi lao la nyongeza ya eneo la kufanya ujenzi huo maeneo ya Jangwani

Katibu mkuu wa Baraza la Wazee wa klabu hiyo Mzee Ibrahim Akilimali amesema wao wamekabidhiwa jukumu hilo na baada ya kusubiri majibu kwa muda mrefu ndipo wameamua kuchukua uamuzi huo wa kwenda kwa mkuu wa mkoa na kumpelekea barua ya kumkumbusha juu ya ombi la klabu hiyo.

Wazee hao wanataraji kutimiza azma hiyo May 19 siku ya Jumatatu na watamwomba mkuu wa mkoa kuwapa majibu kabla ya mkutano mkuu wa klabu hiyo utakaofanyika Juni mosi ili uongozi wa timu hiyo uwe na jibu la kuwapa wanachama wao.