Jumanne , 12th Apr , 2016

Baada ya kukamilisha majukumu yao ya kimataifa wakiwakilisha Tanzania katika michuano ya vilabu barani Afrika timu za Yanga SC na Azam FC kesho wanarejea katika mshike mshike wa michuano ya ligi kuu bara wakiwa katika viwanja tofauti hapa nchini.

Logo ya ligi kuu ya soka Tanzania bara VPL.

Ligi Kuu ya soka Tanzania bara VPL inatarajiwa kuendelea kesho Jumatano, kwa michezo miwili ya viporo kuchezwa katika viwanja vya Manungu Turiani mkoani Morogoro na uwanja wa Taifa jijini Dar es salaam.

Michezo hiyo ya viporo ni baina ya mabingwa watetezi wa ligi kuu hiyo timu ya Young Africans wanaoshika nafasi ya pili kwenye msimamo wa ligi hiyo ambao watakuwa wenyeji wa wachimba migodi kutoka Shinyanga timu ya Mwadui FC inayokamata nafasi ya sita katika uwanja wa Taifa jijini Dar es salaam.

Mchezo mwinginine wa hiyo kesho ni kiporo cha tatu kwa Azam fc ambapo Wakata miwa wa Turiani, Mtibwa Sugar walio katika nafsi ya nne katika msimamo wa ligi kuu watawakaribisha wanarambaramba hao Azam FC walio juu yao katika nafasi ya tatu, mchezo utakaochezwa katika uwanja wa Manungu Turiani mkoani Morogoro.

Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), limewapongeza viongozi, mashabiki, wachezaji wa vilabu na timu za Taifa kwa kufanya vizuri katika michezo mbalimbali ya kimataifa iliyochezwa mpaka sasa.

Katika kipindi cha mwezi mmoja, Tanzania imeshiriki katika michuano mbalimbali ya kirafiki, mashindano ngazi za vilabu, timu za taifa ikiwemo ya Wanawake (Twiga Stars), Vijana (Serengeti Boys) na Taifa Stars.

Katika michezo kumi iliyochezwa mfululizo mpaka sasa, timu za Tanzania hazijapoteza mchezo hata mmoja mpaka sasa, ikiwa ni kwa vilabu pamoja na timu za taifa za Wanawake, Vijana na Taifa Stars.

Twiga Stars ilitoka sare ya bao 1- 1 dhidi ya Zimbabwe mchezo uliochezwa Harare, Yanga ikaifunga APR mjini Kigali 2-1, kabla ya kutoka sare ya bao 1-1 jijini Dar es salaa, wakati Azam FC ilifunga Bidvest 3-0 Johanesburg na kuendeleza tena ushindi wa 4-3 Azam Complex Chamazi.

Taifa Stars ikiwa mjini N’Djamena ilibuka na ushindi wa bao 1-0 dhidi ya Chad katika mchezo wa kuwania kufuzu AFCON 2017, Serenegti Boys ikiifunga The Pharaohs kutoka Misri katika michezo miwili ya kirafiki ya kimataifa (2-1), (3-1) michezo iliyochezwa Uwanja wa Taifa na Azam Complex Chamazi.

Mchezo wa tisa wa kimataifa, Yanga SC ilitoka sare ya bao 1-1 dhidi ya Al Ahly katika mchezo wa Ligi ya Mabingwa Afrika (CAF CL), huku Azam FC ikiibuk na ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya Esperance ya Tunisia katika mchezo wa Kombe la Shirikisho barani Afrika (CAF CC).

TFF inawaomba wachezaji, viongozi, wadau na Mashabiki kuendelea kupigana kusaka ushindi katika michezo inayofuata na kuipeperusha vyema bendera ya Tanzania nje ya nchi.