Jumatano , 22nd Jan , 2020

Kocha wa zamani ya klabu ya Yanga, Mwinyi Zahera ameeleza sababu nyingine iliyopelekea kuachana na timu hiyo kuwa ni ujio wa kocha Charles Boniface Mkwasa.

Kocha Zahera na Charles Boniface Mkwasa

Zahera amesema hayo alipokuwa akihojiwa na kipindi cha Kipenga Xtra cha East Africa Radio, ambapo amesema alikubali kuachana na Yanga baada ya kuambiwa kuwa awe tayari nafasi ya kocha wake msaidizi, Noel Mwandila ichukuliwe na Charles Mkwasa.

"Uongozi waliniambia nikubali kumtoa kocha wangu msaidizi Noel Mwandila ili aje Mkwasa, lakini sikukubali kwasababu sikuona sababu yoyote ya kumuondoa Mwandila, ingekuwa ni kumkosea Mungu", amesema Zahera.

"Mimi nilikataa Mkwasa awe chini yangu kwa sababu yeye namuheshimu ni kocha mkubwa na nilipofika Yanga, yeye ndiye alinisainisha mkataba sasa ingekuwaje mimi nimtume?. Halafu tulikuwa tunapishana kiufundi, alikuwa anaamini vitu tofauti na mimi", ameongeza.

Aidha Zahera ameishauri Yanga kuwa isimuweke Mkwasa katika benchi la ufundi la timu na badala yake imuajiri kama Mkurugenzi wa Ufundi kutokana na heshima na utaalamu alio nao na kumuacha kocha mkuu afanye kazi na kocha msaidizi anayemtaka.