Jumanne , 11th Oct , 2016

Serikali imesema kuwa Tanzania inapoteza takriban hekta 372,000 za uoto wa asili, upotevu ambao unachangiwa kwa kiasi kikubwa na shughuli za binadamu katika maeneo yaliyotengwa kwa ajili ya hifadhi.

Mhandisi Ramo Makani - Naibu Waziri Maliasili na Utalii

Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii Mhandisi Ramo Makani amesema serikali kupitia wizara yake imeanza kutafuta ufumbuzi wa tatizo la wananchi la kufanya uvamizi katika maeneo hayo.

Mhandisi Makani ameyasema hayo leo Jijini Dar es Salaam wakati akifafanua kuhusu uondoaji wananchi katika maeneo ya hifadhi na kuongeza kuwa katika kipindi hiki ambacho serikali inaendelea kutafuta ufumbuzi wa kudumu na endelevu wa migogoro ya ardhi wananchi wanapaswa kufuata sheria na kuacha tabia ya kuvamia maeneo ya hifadhi.

Amewataka viongozi wanaohusika katika maeneo hayo wasiwabughudhi wanachi na badala yake wazingatie taratibu katika kutekeleza sheria katika kushughulikia ukiukwaji wa sheria kwa wananchi waliopo katika vitongoji na vijiji vilivyosajiliwa.

Pamoja na mambo mengine Mhandisi Makani pia amepiga marufuku uanzishwaji wa shuguli mpya katika maeneo ya hifadhi hizo.