Jumatano , 3rd Jun , 2020

Waziri wa Elimu Sayansi na Teknolojia Prof Joyce Ndalichako ametoa muda wa hadi kufika Ijumaa wiki hii ambayo itakuwa Juni 5, 2020, vyuo vyote vya elimu ya juu hapa nchini viwe vimemaliza kuwapa fedha za kujikimu wanafunzi wote na si vinginevyo.

Amesema hayo leo Juni 6, 2020 wakati akizungumza baada ya kukabidhi magari manne kwa chuo cha taifa cha usafirishaji (NIT).

Ndalichako amesema, ''serikali haitakuwa na mswalia mtume katika hili kwa kuwa tayari ilishatoa fedha hizo na hakuna sababu ya kuchelewa kuwapa wanafunzi fedha hizo''.

Kwa upande wake makamu mkuu wa chuo cha taifa cha usafirishaji NIT Mhandisi Prof Zacharia Mganilwa amesema magari waliyokabidhiwa leo yanakwenda kutumika kwenye shughuli za uendeshaji wa chuo.

Vyuo vimefunguliwa Juni 1, 2020 baada ya kusimama kwa takribani miezi mitatu kutokana na janga la Corona. Serikali tayari imeshathibitisha kuingiza fedha za mikopo kwa wanafunzi hivyo kuacha jukumu kwa vyuo kukamilisha kuwapatia wanafunzi.