Sunday , 2nd Dec , 2018

Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mhe. Kangi Lugola ameliagiza Jeshi la Magereza mkoani Arusha kuanza upya ujenzi wa kiwanda cha kisasa cha samani cha jeshi hilo ambacho kiliungua moto mwezi uliopita.

Waziri Kangi Lugola akifanya ukaguzi wa kiwanda cha samani cha Jeshi la Magereza Jijini Arusha

Kangi ameyasema hayo wakati alipotembelea kiwanda cha hicho kilichopo Jijini Arusha hii leo, Jumapili, Desemba 02 ambapo amempa maelekezo Kamishna Jenerali wa Magereza, (CGP) Phaustine Kasike kuhakikisha kiwanda hicho kinajengwa haraka.

Waziri huyo wa Mambo ya Ndani pamoja na watendaji wake, akiwemo Naibu Waziri, Mhandisi Hamad Masuni pamoja na Katibu Mkuu, Ramadhan Kailima wapo katika ziara mbalimbali nchini wakitembelea miradi mbalimbali na vituo vya Polisi na Magereza.

Katika hatua nyingine, akiwa Jimboni kwake, Mwibara, Wilaya ya Bunda mkoani Mara, Novemba 29, Kangi aliwataka watu wote wanaojihusisha na ujambazi wajisalimishe pamoja na silaha zao, akisisitiza kuwa Polisi hawatalala mpaka wamtie mbaroni jambazi wa mwisho.