Wednesday , 9th Aug , 2017

Rapper wa kike kwenye game ya bongo fleva TammyThe Baddest, amesema maisha ambayo anaishi yaliyomfanya baba yake amkatalie kufanya muziki, lakini amefanikiwa kumshawishi japo hataki kumtambua mwanaye pindi anapokuwa jukwaani.

Msanii Tammy the Baddest

Akipiga stori kwenye Planet Bongo ya East Africa Radio, Tammy amesema akiwa nyumbani anabaki kuwa yule mtoto wa baba yake ambaye anaenda mpaka msikitini kuabudu, lakini akiwa kwenye kazi zake hata baba yake hamjui The Baddest.

"Nikiwa nyumbani lazima niwe na baibui na madera, lakini nikiwa kwenye kazi zangu nakuwa The Baddest, ndiyo maana baba yangu ilichukuwa muda mrefu sana kunikubalia kufanya muziki Ila kitu kizuri yule anayemuona kwenye Tv ni tofauti kabisa na binti yake, binti yake ni yule yule ambaye yeye ametaka awe hivyo, yule the baddest hata hajui ametokea wapi", alisema Tammy.

Tammy aliendelea kusema kuwa kitendo cha yeye kuwa msanii hakimzuii kuishi maisha yake ya kawaida, kwani hata marafiki zake wakubwa ni wauza mitumba na madereva boda boda.

"Haya ndio maisha yangu, bajaji, boda boda, wauza chips, Karume wauza mitumba ndiyo watu wangu", alisema Tammy.