Friday , 19th Jan , 2018

Vinara wa ligi kuu soka Tanzania Bara Simba SC jana ilimtangaza kocha mkuu mpya Pierre Lechantre ambaye ana sifa ya kumfundisha mshambuliaji wa zamani wa Cameroon Samuel Eto'o.

Kocha huyo raia wa Ufaransa anachukua mikoba ya Mcameroon Joseph Omog amabye alikuwa anatokea taifa ambalo anatoa Eto'o na taifa ambalo lilipewa ubingwa wa Afrika mwaka 2000 na Pierre Lechantre akiwa kocha mkuu.

Pierre Lechantre akiwa na umri wa miaka 52 alikuwa akimfundisha kijana mdogo wa miaka 19, akifahamika kama Samuel Eto'o Fils ambaye alikuwa sehemu ya kikosi cha Cameroon kilichotwaa ubingwa wa AFCON mwaka 2000.

Wachezaji wengine wenye majina makubwa aliowafundisha kocha huyo kwenye kikosi cha Cameroon ni nahodha wa taifa hilo kwa wakati huo Rigobert Song, Marc-Vivien Foé pamoja na Patrick M'Boma.

Katika mchezo wa fainali uliowakutanisha wenyeji Nigeria dhidi ya Cameroon, Eto'o alifunga bao la mapema dakika ya 26 kabla ya  M'Boma kuongeza bao la pili dakika ya 31. Lakini baadae Nigeria walisawazisha na Cameroon kushinda kwa Penalti.

Pierre Lechantre alizaliwa April 2, 1950 mjini Lille nchini Ufaransa. Nov 16, 2016  kocha huyo alifukuzwa kazi na Congo Brazzaville baada ya timu ya taifa hilo kukubali kichapo cha bao 1-0 kutoka kwa Uganda kwenye michuano ya kuwania kufuzu Kombe la dunia.