Saturday , 29th Apr , 2017

Kocha msaidizi wa Yanga SC, Juma Mwambusi amewatoa wasiwasi mashabiki zao kwa kuwa hakikishia kupata ushindi wa pointi 3 katika mechi yao ya kesho (Jumapili) dhidi ya Mbao FC inatakayochezwa katika uwanja wa CCM Kirumba jijini Mwanza.

Kocha msaidizi wa Yanga SC, Juma Mwambusi

Mwambusi amesema kwa sasa mkakati wao mkubwa ni kuhakikisha wanapambana vilivyo ili timu yake iweze kusonga mbele katika michuano hiyo ambayo Yanga ndiyo mabingwa watetezi japokuwa wakionekana na pengo kubwa katika safu ya ushambuliaji kwa kumkosa Donald Ngoma pamoja na Vincent Bossou.

“Tunashukuru tumefika Mwanza salama na tunashukuru wadau na wapenzi wa klabu yetu kwa kutupokea vizuri, wachezaji wanaari kwa ajili ya kupambana na kuhakikisha wanashinda....Tunajua tuna kibarua kigumu mbele yetu lakini sisi lengo letu ni kuhakikisha tunashinda mchezo wetu". Alisema Mwambusi

Pamoja na hayo, Nahodha wa kikosi hicho Nadir Haroub 'Canavaro' amesema timu yao iki tayari kutetea taji lao lisipotee kwenda katika vilabu vingine.

“Ili kutimiza malengo yetu ni lazima tupambane tuhakikishe tunashinda na kufika fainali kwani tumedhamiria kuchukua makombe yote msimu huu na kwa sasa matatizo ya uongozi tumeyaweka pembeni na tulichodhamiria sasa ni kuhakikisha tunapambana na kucheza mpira". Alisema Canavaro.

Kwa upande mwingine mechi hiyo itakuwa ya pili kwa timu hizo mbili kukutana, baada ya ile ya mzunguko wa kwanza wa Ligi Kuu Bara kuisha kwa Yanga kushinda mabao 3-0.