Wednesday , 23rd Jul , 2014

"Hofu ya kucheza mechi za kimataifa kulitugharimu. Tulikuwa tunawaogopa wapinzani, lakini kadri muda ulivyozidi kwenda tukawa tunawazoea kidogokidogo. Mechi ya marudiano hatutokuwa na hofu tena".

Omar Wayne-Nahodha wa Serengeti Boys.

Nahodha wa timu ya taifa ya vijana chini ya miaka 17, Omar Wayne, amesema hofu ya mechi ya kimataifa kuliwasababishia kukosa utulivu uliowafanya wakashindwa kuutumia vizuri uwanja wa nyumbani na kujikuta wakitoka sare ya 0-0 dhidi ya wenzao wa Amajimbos wa Afrika Kusini.

Mchezo huo wa kwanza wa hatua ya mtoano ya mzunguko wa pili kuelekea fainali za mataifa ya Afrika kwa umri huo, ulifanyika Julai 18 mwaka huu ma uliisha kwa sare ya 0-0 huku Serengeti wakipoteza nafasi kadhaa za wazi mojawapo ikipotezwa na yeye mwenyewe Omar Wayne ambapo amejitetea kwa kusema alitaka 'kuukata' mpira ule uzunguke katika umbo la ndizi lakini kwa bahati mbaya haukwenda kama alivypanga na kujikuta akimpasia kipa. Hata hivyo, hakusita kumpongeza kipa wa Amajimbos Mondili Mpoto aliyeonesha utulivu kwenye kuokoa mpira ule.

"Nimefunga mabao mengi kama yale, mazoezini na kwenye baadhi ya mechi. lakini siku ile mpira ulikaa kukunjika kama ambavyo huwa inakuwa na pia kipa wao aliniotea kwa kunihesabia hatua hivyo kuudaka mpira ule." amesema Wyne

Timu hiyo imeingia kambini kujiandaa na mechi ya marudiano itakayofanyika tarehe 27 mwezi huu nchini Afrika Kusini. Mshindi wa mechi hii atacheza na mshindi kati ya Misri na Jamhuri ya Congo ambao mechi yao ya kwanza, Misri walishinda 1-0.

Atakayeshinda hapo atafuzu kwa fainali za 16 za michuano hiyo zitakazofanyika nchini Niger kuanzia tarehe 15 February mpaka tarehe 1 March mwakani.