Monday , 31st Dec , 2018

Kocha wa Yanga Mwinyi Zahera ameweka wazi makombe ambayo ni vipaumbele kwake na klabu huku katika hayo akiiondoa Mapinduzi Cup na ameeleza kuwa hatopeleka kikosi cha kwanza kwenye michuano hiyo.

Kocha wa Yanga Mwinyi Zahera (katikati).

Akiongea leo na wanahabari Zahera amesema kama klabu ni lazima wawe na vipaumbele na wakitaka kushiriki kikamilifu katika kila kombe basi watajikuta wanakosa yote hivyo kipaumbele chake ni ligi kuu na kombe la shirikisho.

"Kufuatana na nguvu yetu tulionayo kwa maana ya wachezaji, inatubidi tuangalie wapi tutapata faida, tupo na ligi kuu, tupo na Azam federation Cup, Mapinduzi cup na Sport Pesa kwahiyo sisi kama yanga tuwe na malengo kwenye kitu chenye manufaa kwetu'', amesema.

Aidha ameongeza kuwa ''tukiamua kuyataka makombe yote tunaweza kosa yote hivyo lazima baadhi ya wachezaji wapumzike kwaajili ya ligi na ASFC".

Hata hivyo Zahera hajataja wachezaji gani wa kikosi cha kwanza hawatakwenda visiwani Zanzibar kwaajili ya michuano hiyo inayoanza kesho Januari 1 na kumalizika Januari 13, 2019.