Tuesday , 31st Jan , 2017

Kamati ya Ulinzi na Usalama mkoani Morogoro ikiongozwa na Mkuu wa Mkoa wa Morogoro DK. KEBWE STEVEN KEBWE inawashikilia watu 13 wakiwemo wakulima  na  wafugaji  wilayani Malinyi  kutokana na kukaidi agizo la serikali

Mkuu wa Mkoa wa Morogoro Stephen Kebwe (Kushoto) akiongoza kamatakamata

Agizo hilo ni la kusitisha shughuli za  kibinadamu  zinazoendelea kufanyika eneo la Kinga katika bonde la mto Kilombero.

Kamati hiyo imewakamata watu hao pamoja na  matrekta sita  na gari moja  mara baada ya kutembelea eneo hilo maalum lililotengwa na serikali na kukuta watu hao wakiendelea   kufanya shughuli  za  kibinadamu ikiwemo  kilimo, ufugaji  na  uvuvi haramu.

Eneo  hilo hifadhi ya bonde la mto Kilombero limetengwa na serikali kwa ajili ya hifadhi mwaka 2012, lakini bado jitihada hizo hazikuleta mafanikio baada ya baadhi ya wananchi kurudi katika eneo hilo na kuendelea kufanya  shughuli za kibinadamu ndani ya eneo la kinga.

Kulingana na hali hyo Dkt. Kebwe amezitaka Halmashauri za Wilaya tatu za kilombero, Ulanga na Malinyi ambazo zinapakana na mto huo kufanya ufuatiliaji wa karibu katika kuhifadhi bonde hilo.

Hata hivyo, Dkt. Kebwe ameagiza kufikishwa kwenye vyombo vya sheria wale wote waliokamatwa katika zoezi hilo ili wawe mfano kwa wananchi wenye tabia hiyo ya kukaidi maagizo ya Serikali.

Amesema, zoezi hilo la kamata kamata katika bonde  la mto kilombero litakuwa endelevu na matrecta yaliyokamatwa yatapelekwa kituo cha polisi na wamiliki wa zana hizo wataitwa ili kujibu tuhuma zinazowakabili za kufanya shughuli za kilimo katika eneo hilo ambalo limepigwa marufuku.