Tuesday , 10th Dec , 2019

Mwenyekiti wa klabu ya Yanga, Dkt. Mshindo Msolla ametoa ufafanuzi juu ya mapato na matumizi ya klabu hiyo tangu uongozi wake ulipoingia madarakani, Juni 2019, huku akibainisha uwepo wa madeni ambayo wamerithi kutoka kwa uongozi uliopita.

Mwenyekiti wa Yanga Mshingo Msolla (suti ya kijivu waliokaa) akiwa na mashabiki wa Yanga.

Msolla amesema gharama za kuendesha timu ni kubwa, kuliko mapato yanayoingia, huku wakiwa wamerithi madeni makubwa kutoka katika uongozi uliopita ambayo inabidi yalipwe au kupunguzwa kadri inavyowezekana.

"Nimeamua kuja kwenu Waandishi ili nitoe ufafanuzi juu ya mapato na matumizi ya klabu yetu. Tulivyoingia madarakani tulikuta timu madeni makubwa ambayo tumejitahidi kuyapunguza huku bado tukitakiwa kuiendesha timu", alisema Msolla.

Mwenyekiti huyo ametaja madeni makubwa ya aina nne waliyorithi kama ifuatavyo:-

1. Serikali (Mamlaka ya Mapato Tanzania 'TRA' shilingi milioni 800), 

2.Ada ya uhamisho ya wachezaji waliosajiliwa miaka miwili iliyopita shilingi milioni 254.

3. Madeni ya makocha na wachezaji waliopita (Hans Van Pluijm, George Lwandamina, Youthe Rostand, Donald Ngoma na Obrey Chirwa) jumla shilingi milioni 600.

4. Watu binafsi shilingi milioni 237

5. Gharama za Usajili wa timu za wakubwa na ile ya Wanawake shilingi milioni 600.

Msola ametaja vyanzo vya mapato vya klabu hiyo ambayo ni SportPesa, KCB, Vodacom, Azam TV, GSM, Yanga TV na kampuni ya Maji ya Afya, ambayo kwa mwaka wanapata shilingi bilioni mbili wakati gharama za kuiendesha timu ni Bilioni nne.

Aidha Msolla amewaahidi wanachama wa timu hiyo kuwa, mpaka Mei 2020, watakuwa wameingia katika mfumo wa uwekezaji kwa njia ya hisa. Amesema watawashirikisha Wanachama katika kila hatua ili maamuzi yawe ya watu wote.